Select your language

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imeipongeza Serikali ya Awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kusimamia mapinduzi makubwa yenye kuongeza zaidi ufanisi katika Bandari. 

Pongezi hizo zimetolewa tarehe 14 Juni, 2025 na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Dkt.Joseph Mhagama (Mb) kwa niaba ya kamati yake baada ya kutembelea na kukagua Shughuli za utekelezaji katika Bandari. 

“ Kamati imejiridhisha na utendaji kazi katika Bandari ya Dar es Salaam na kimsingi ziara imewezesha Waheshimiwa Wabunge kuwa na uelewa Mpana wa majukumu ya Bandari na marekebisho ya Sheria ambayo yanapofanyika yanaleta tija kwa Taifa. Pongezi nyingi kwa Serikali na Mhe. Rais Dkt Samia Suluhu Hasaan Kwa mapinduzi haya makubwa yenye kuleta Ufanisi katika Bandari.” Amesema Mhe.Dkt. Mhagama. 

Pia kamati imeipongeza Menejimenti ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) kwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu na kuhakikisha huduma bora zinatolewa kwa Wateja, Wadau na Umma kwa ufanisi na kwa wakati sahihi

Akijibu hoja za Wajumbe wa Kamati hiyo kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi, Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe.David Kihenzile(Mb) ameishukuru Kamati hiyo ambayo kimsingi inahusika hasa na masuala ya kisheria na kisera kwa kufanya ziara hiyo iliyowawezesha kuona na kupata uelewa mpana kuhusu Shughuli za utekelezaji Bandarini, huku akiihakikishia kamati kuwa maelekezo, maoni na ushauri wao utafanyiwa kazi. 

Mapema akitoa wasilisho la utendaji wa Bandari na utekelezaji wa miradi ya uboreshaji na upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam mbele ya kamati kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mbossa, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dkt. Baraka Mdima, amesema hadi sasa kukamilika kwa utekelezaji wa mradi katika baadhi ya maeneo kumeleta manufaa mbalimbali ikiwemo kuongezeka kwa uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam kuhudumia Meli kubwa zenye kubeba makasha hadi 8,000, kuongezeka uwezo wa kuhudumia shehena kutoka tani milioni 16 kabla ya maboresho hadi kufikia tani milioni 30 za  sasa na hivyo kuongeza mapato ya Serikali huku ikihudumia eneo lenye ukubwa wa soko lenye takribani watu milioni 700 na kuongeza uwezo wa kiushindani kati ya Bandari ya Dar es Salaam na Bandari nyingine za kikanda. 

Kwa sasa TPA inatekeza mradi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam (DMGP) unaogharimu Shilingi Trilioni 1.118 ambazo ni Fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia, Fedha za msaada kutoka kwa Wafadhili na mapato ya ndani ya TPA huku ikikamilisha awamu ya kwanza ya Upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa ujenzi wa gati mpya namba 12-15.