Na Mwandishi Wetu
Ushirikiano kati ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) na Bandari ya Antwerp ya nchini Ubelgiji umepangwa kuimarishwa zaidi ili kuongeza tija na kufungua fursa zaidi za uwekezaji Bandarini.
Hayo yamebainika hivi karibuni mara baada ya ujumbe wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Ubelgiji na Wawekezaji wa Bandari ya Antwerp kufanya ziara katika Bandari ya Dar es Salaam.
Akizungumza wakati wa ziara ya ujumbe, Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Bw. Plasduce Mbossa amesema ziara ya ujumbe huo umelenga kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya TPA na Bandari ya Antwerp.
Bw. Mbossa pia ametumia fursa hiyo kuelezea fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo katika Bandari zinazosimamiwa na kuongozwa na Mamlaka.
Maeneo mengine yatakayoguswa na ushirikiano huo, ni pamoja na maboresho ya huduma za Kibandari kulingana na Mkataba wa ushirikiano wa Bandari hiyo ya Antwerp na TPA.
Ushirikiano huo pia umelenga kujikita katika kutoa ushauri elekezi wa namna bora zaidi ya kuyafikia mabadiliko chanya ya huduma za Kibandari hapa nchini, pamoja na ushirikiano wa karibu na Jumuiya hiyo.
Aidha mazungumzo yao yamegusia nia njema ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Maboresho ya Bandari Nchini ambapo Bw. Mbossa ameulezea Ujumbe huo kuhusu fursa zilizopo za Uwekezaji katika Bandari za TPA.
Ujumbe wa Jumuiya ya Wafanyabiashara ya Ubelgiji, Wawekezaji na Wafanyakazi wa Bandari ya Antwerp uliofanya ziara bandarini, uliongozwa na Balozi wa Ubelgiji nchini Tanzania, Mhe. Peter Huyghebaert na Balozi wa Tanzania katika Ufalme wa Ubelgiji na Jumuiya ya Ulaya, Mhe. Jestas Abuok Nyamanga ulifanya ziara katika Bandari ya Dar es Salaam kwaajili ya kujionea fursa mbalimbali za uwekezaji katika Bandari hiyo.
Na Mwandishi Wetu
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imeshiriki katika zoezi la uokoaji wa wathirika wa ajali ya Ghorofa liliroporomoka katika kata ya Kariakoo, Wilaya ya Ilala, Jijini Dar es Salaam kwa kutoa msaada wa vifaa mbalimbali vya uokoaji.
TPA imetoa msaada wa vifaa vya uokoaji kama kofia ngumu, vizibao, glovu, na mtambo maalum wa kunyanyua vitu vizito ili kusaidia kazi za uokoaji zinazoendelea katika ajali hiyo.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA, wakati wa kukabidhi vifaa mbalimbali vya uokoaji katika eneo la tukio, Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Abed Gallus, alisema TPA imesikitishwa sana na tukio hilo lililosababisha vifo na majeruhi, na kuwaombea waliopatwa na mkasa huo wapate uponyaji wa haraka.
“TPA, kama wadau wakubwa wa biashara na wafanyabiashara wa Kariakoo na Tanzania kwa ujumla, tumeguswa sana na tukio hili kwa sababu waathirika ni wadau wetu na Watanzania wenzetu,” alisema Bw. Gallus.
Mwandishi Wetu
Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) imeipongeza Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kwa kuendelea kuboresha huduma zake katika Bandari zake na kufanya Wafanyabiashara kuendelea kufurahia huduma na kuendelea kutumia bandari za TPA.
Pongezi hizo zimetolewa tarehe 25 Novemba,2024 kupitia Risala yao iliyosomwa na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo kanda ya Ziwa Victoria Bw. Nicholaus Basimaki, katika Mkutano wa 10 wa mwaka 2024, uliofanyika Ukumbi wa Ubungo Plaza Jijini Dar es Salaam.
TPA ilikuwa ni miongoni mwa Wadhamini wa Mkutano huo wa siku moja umeshirikisha Wajumbe 400 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.
Na Mwandishi Wetu
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imezihakikishia Nchi zinazohudumiwa na Bandari za Tanzania chini ya TPA kuwa, itaendelea kuunga mkono juhudi na jitihada za kuimarisha biashara ya kikanda na kukuza uchumi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA katika ufunguzi wa Mkutano wa tano wa Juma la Shughuli za Kibandari na Forodha “Ports & Customs Week 2024“uliofanyika tarehe 3 hadi 4 Desemba,2024 Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano Dkt. George Fasha, amesema nia hiyo ya TPA inaenda sambamba na ukuaji wa maendeleo ya teknolojia pamoja na matokeo chanya kwa Bandari na mifumo ya forodha na kuimarisha ushirikiano ili kuendeleza na kuwezesha biashara na kukuza uchumi miongoni mwa nchi zinazotumia Bandari za Tanzania.
Mkutano huu wa Shughuli za Kibandari na Forodha ni muhimu kwani unatoa suluhu za kiteknolojia kwa changamoto zinazokabili bandari na mamlaka ya forodha barani Afrika ukiwa unaongozwa na kaulimbiu ya “Kuimarisha Ushirikiano wa Kikanda na Uwekaji mifumo ya Kidijiti wa Mipaka, Bandari na Forodha.
Na Mwandishi Wetu
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Bw. Plasduce Mbossa amesema kuwa wamejipanga kufanya upanuzi wa Bandari za Mamlaka ili kuendelea kutoa huduma shindani katika soko la Afrika na Kimataifa.
Akizungumza hivi karibuni, Mbossa amesema kuwa TPA imejiweka katika nafasi nzuri zaidi ya kiushindani kutokana na uwekezaji wake unaoendelea katika bandari mbalimbali hapa nchini.
Moja ya mikakati hiyo ni pamoja na mpango wa kupanua na kujenga gati 10 katika Bandari ya Dar es Salaam ili kuongeza ufanisi na tija katika bandari hiyo.
“Katika kuhakikisha wateja wetu wanaendelea kupata huduma bora na stahiki sisi kama mamlaka tumekuja na mpango wa kuongeza gati 10 katika bandari ya Dar es salaam,”
“Hii inaenda kupanua soko la biashara kwa watumiaji wa bandari yetu kwani ufanisi utakuwa ni mkubwa na utakidhi mahitaji ya wateja wetu”, amesema.
Aliongeza kusema TPA imeendelea kuboresha miundombinu ya bandari zake ambazo ni pamoja na bandari ya Bagamoyo, Bandari ya Tanga, Mtwara, Mbamba Bay na bandari zingine ambazo ziko chini ya mamlaka hiyo.
Amesema hayo yote yanafanyika ili kuhakikisha kuwa TPA inachochea uchumi wa Taifa kupitia Bandari zake kwa kushirikiana na wawekezaji waliopo.
“TPA tumejipanga kuufungua uchumi wa Taifa kwa kutumia bandari zetu na ndio maana tumeendelea kuboresha maeneo mengi ya bandari zetu ili ziweze kutoa huduma kwa wateja wetu wa ndani na nje ya nchi.”
“Kwa kupitia uwekezaji ambao tumeufanya katika bandari zetu, matunda yake tumeanza kuyaona ambapo hadi sasa kumekuwa na utofauti mkubwa katika huduma za bandari ukilinganisha na miaka kadhaa ya nyuma”
“Hii inatokana na juhudi za Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuleta mageuzi makubwa ya kiutendaji katika bandari zetu ili kuchochea biashara zaidi na kukuza uchumi wa nchi yetun”amesema Bw. Mbossa.
EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"