Wafanyakazi wa Bandari ya Tanga wamemchagua Bw. Aliko Mwakipagala kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari (DOWUTA) tawi la Tanga, huku Bw. Iddi Mfaume Bode akichaguliwa kuwa Katibu wa tawi hilo.
Pia katika Mkutano huo wa uchaguzi, Wafanyakazi waliwachagua wawakilishi mbalimbali kuunda Kamati ya Utendaji ya DOWUTA tawi la Bandari ya Tanga.
Aidha akifungua mkutano huo wa uchaguzi, Meneja wa Bandari ya Tanga, Bw. Salehe Mbega, alitoa rai kwa wafanyakazi wa Bandari ya Tanga kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha ufanisi unaendelea kunapatikana katika bandari hiyo.
Akiongea katika Mkutano huo Bw. Mbega amesema, ufanisi unaoonekana katika bandari hiyo ni pamoja na utendajikazi uliotukuka kutoka kwa wafanyakazi hivyo, aliwataka kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili tuendelee kuvuka malengo ya kila mwaka yanayotolewa na serikali.
“Bandari ya Tanga imeendelea kuvutia wadau mbalimbali kutaka kufanyakazi na sisi hii yote ni kutokana na tunavyofanya kazi vizuri hivyo nawaomba tuendelee kuwajibika ipasavyo ili mwisho wa siku tufaidike kwa kujituma kwetu”. Aliongeza Bw. Mbega
Aidha Bw. Mbega aliwahakikishia wafanyazi hao changamoto zote zitaendelea kufanyiwa kazi kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi ikiwa ni pamoja na kuendelea kuboresha maslahi.
Katika hatua nyingine Bw. Mbega aliwatakia heri wanachama na wagombea wote waliotia nia katika uchaguzi huo na kuwataka kwenda kusimamia maslahi ya wafanyakazi pamoja na mambo muhimu yaliwekwa kwa kuzingatia sheria na kanuni za utumishi.
Awali akimkaribisha Meneja huyo, Mwenyekiti wa muda wa DOWUTA Tawi la Tanga aliyekuwa anamaliza muda wake Bw. Aliko Mwakipagala alimhakikishia Bw. Mbega kuwa chama hicho kitaendelea kutoa ushirikiano kwa uongozi wa bandari ili kuhakikisha malengo katika uhudumiaji wa shehena yanafanikiwa.
Katika kipindi cha kwanza Mwakipagala alishikia nafasi ya Mwenyekiti baada ya aliyekuwa Mwenyekiti Bw. Ali Sankole kustaafu utumishi wake bandarini.



Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi hiyo IGP Mstaafu Mhe. Balozi Ernest Mangu, imetembelea Bandari ya Tanga kwa lengo la kujionea hali ya Utendaji katika bandari hiyo.
Bodi hiyo ilipokelewa na Naibu Mkurugenzi Mkuu Mha. Dkt. Baraka Mdima kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mbosa, na kupokea taarifa ya utendaji kazi wa Bandari ya Tanga.
Akiongea katika ziara hiyo Mhe. Balozi Mangu, amesema maboresho makubwa ya miundombinu yaliyofanywa na Serikali katika Bandari nchini ikiwemo Bandari ya Tanga, yataleta manufaa makubwa kiuchumi na kubadili maisha ya Watanzania na kuhudumia pamoja na nchi jirani.
Aidha Bodi hiyo imeiagiza Menejimenti ya TPA kuendelea na mikakati yake ya kutwaa maeneo yaliyopo karibu na Bandari ya Tanga ili kukabiliana na uhaba wa nafasi ya kuhifadhia shehena ya mizigo ambayo imekuwa inaongezeka mwaka hadi mwaka katika bandari hiyo.
Awali akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Bandari, Meneja wa Bandari ya Tanga, Bw. Salehe Mbega amesema, kwa kipindi cha miezi sita ya mwaka wa fedha 2025/2026 imevuka malengo katika kuhudumia meli, shehena na ukusanyaji wa mapato. Mafanikio hayo yametokana na maboresho yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Bodi hiyo pia ilikutana na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Buriani, ofisini kwake, ambaye alitoa pongezi kwa Bandari ya Tanga kwa jinsi inavyoshirikiana na serikali ya Mkoa wa Tanga na kuwa na utendaji bora wenye kuvuka malengo katika kuhudumia meli, shehena ya mizigo na ukusanyaji wa mapato.
Katika ziara hiyo, Bodi ya Wakurugenzi wa TPA ilitembelea Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta ghafi la EACOP katika eneo la Chongoleani.



Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Bw. Plasduce Mkeli Mbossa, ametunukiwa Cheti cha Heshima kwa usimamizi wake ikiwa ni kutambua na kuthamini mchango wangu wake mkubwa na utoaji huduma wa kipekee kwa jumuiya ya kimataifa ya Forodha, katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Forodha 2026.
Cheti hicho cha kimetolewa na Shirika la Forodha Duniani (WCO) kwa niaba ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), katika maadhimisho yaliyofanyika tarehe 26 Januari, 2026, jijini Dar es Salaam, chini ya kaulimbiu isemayo:
“Forodha inalinda jamii kupitia umakini na uwajibikaji.”
Cheti hicho cha heshima kimetolewa ikiwa ni kuthamini huduma ya kipekee ya TPA chini ya usimamizi wa Bw. Mbossa na mchango mkubwa katika kuunga mkono na kuimarisha jumuiya ya kimataifa ya Forodha, hususan kupitia uboreshaji wa mifumo, taratibu na ushirikiano wa taasisi.
Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Forodha 2026 yalilenga kutambua na kuenzi mchango wa sekta ya forodha katika kukuza biashara halali, kulinda uchumi wa taifa, kuongeza makusanyo ya mapato ya serikali, pamoja na kuimarisha uwajibikaji na ushirikiano kati ya TRA na wadau wake wakuu, wakiwemo taasisi zinazosimamia bandari na biashara ya kimataifa.
Akizungumza kabla ya kukabidhi cheti hicho, Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Yusuph Juma Mwenda, aliipongeza TPA kwa ushirikiano wake wa karibu na wa muda mrefu na TRA, uliosaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha ufanisi wa shughuli za forodha bandarini, kurahisisha biashara na kuimarisha udhibiti wa mapato ya serikali.
Bw. Mwenda alieleza kuwa TPA imeendelea kuwa mdau muhimu na mfano wa kuigwa, kwa kuzingatia misingi ya weledi, uwajibikaji na uadilifu, huku ikiendelea kushirikiana kwa karibu na TRA katika utekelezaji wa maboresho ya mifumo na taratibu za forodha kwa manufaa ya taifa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Bw. Plasduce Mkeli Mbossa, ameishukuru TRA na Utawala wa Forodha wa Tanzania kwa kutambua mchango wake binafsi na wa taasisi ya TPA kwa ujumla, na kuahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano uliopo ili kuongeza ufanisi wa bandari na kuchangia zaidi katika ukuaji wa uchumi wa nchi.
Bw. Mbossa amesema kuwa tuzo hiyo ni chachu kwa TPA kuendelea kuboresha huduma zake, kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kisasa, pamoja na kudumisha misingi ya uwajibikaji, uwazi na uadilifu katika utoaji wa huduma za bandari na forodha.
Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Forodha yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kutathmini mafanikio ya sekta ya forodha, kuimarisha mahusiano na wadau wa biashara, pamoja na kuweka mwelekeo wa pamoja wa kuboresha mazingira ya biashara na maendeleo ya taifa kwa ujumla.



Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Abed Gallus Abed, tarehe 23 Januari, 2026, amekutana na wadau wa bandari kujadili masuala mbalimbali yanayohusu shughuli za kibandari za kila siku, kwa lengo la kuongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam na kuhakikisha malengo ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2025/2026 yanafikiwa.
Kikao hicho cha siku moja, ambacho hufanyika kila mwezi, huwakutanisha Menejimenti ya Bandari ya Dar es Salaam na wadau wake wakuu, ambapo hukaa meza moja kujadiliana kwa kina masuala yanayolenga kuboresha utoaji wa huduma za kibandari, hatua inayochangia kuongeza ufanisi katika uhudumiaji wa shehena na kurahisisha biashara.
Katika kikao hicho, wadau walipata fursa ya kubadilishana mawazo, kutoa maoni na mapendekezo juu ya namna ya kuimarisha uratibu wa shughuli za bandari, kuondoa changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku, pamoja na kuboresha ushirikiano kati ya taasisi zinazohusika na mnyororo wa usafirishaji na biashara.
Baadhi ya wadau waliohudhuria kikao hicho ni Waendeshaji wa Bandari DP World Dar es Salaam Limited na Tanzania East Africa Gateway Terminal (TEAGTL), Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (TATOA), Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Vyombo vya Usalama, Chama cha Mawakala wa Meli Tanzania (TASAA) pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Menejimenti ya Bandari ya Dar es Salaam imeendelea kusisitiza umuhimu wa mikutano hiyo ya mara kwa mara kama jukwaa la kujenga ushirikiano, kuongeza uwazi, na kuweka mikakati ya pamoja ya kuboresha ufanisi wa bandari kwa manufaa ya taifa na wadau wa biashara kwa ujumla.


Dar es Salaam — Maboresho makubwa ya miundombinu ya bandari nchini, hususan Bandari ya Dar es Salaam, yameendelea kuleta matokeo chanya kwa kuongeza mapato ya Serikali, ufanisi wa utoaji huduma na kuvutia idadi kubwa ya watumiaji kutoka nchi jirani, huku Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ikiongoza kwa kutumia huduma za bandari hiyo.
Akizungumza wakati wa ziara ya kutembelea Bandari ya Dar es Salaam kama sehemu ya kuelezea mafanikio ya siku 100 za Rais Samia Suluhu Hassan katika sekta mbalimbali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, amesema maboresho hayo yamechochea ukuaji wa uchumi na kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango kuu la biashara kwa ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Bw. Msigwa amesema uwekezaji uliofanywa umeongeza ufanisi katika ubebaji na usafirishaji wa shehena kwenda nchi jirani, hali iliyosaidia kupunguza muda wa meli kukaa bandarini na kuongeza ushindani wa bandari za Tanzania kikanda na kimataifa.
Ameeleza kuwa Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kimkakati kuboresha bandari, kwa lengo la kukuza biashara, kufungua fursa za uwekezaji na kuhakikisha bandari zinachangia kikamilifu ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kijamii.
Kwa mujibu wa takwimu za mwaka wa fedha 2024/2025, bandari za Tanzania zimehudumia shehena kubwa kwa nchi jirani ambapo DRC imeongoza kwa tani 5,995,293, ikifuatiwa na Zambia tani 3,510,706, Rwanda tani 1,724,370, Malawi tani 675,200, Burundi tani 425,774, Uganda tani 185,625, Zimbabwe tani 61,306 na nchi nyingine tani 38,512.
Katika kuimarisha ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam, TPA ilisaini mikataba ya upangishaji na uendeshaji na kampuni za DP World MEA FZE na Adani International Ports Holdings Pte Limited, ambazo zilianzisha kampuni za DP World Dar es Salaam Limited na Tanzania East Africa Gateway Terminal Limited (TEAGTL) kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo.
Bw. Msigwa amesema hadi kufikia Juni 2025, DP World imewekeza takribani Shilingi bilioni 214.2 katika ununuzi wa mitambo mipya, matengenezo ya mitambo ya TPA, usanifu wa mifumo ya kisasa ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), ukarabati wa karakana na uboreshaji wa maeneo ya kuhifadhi shehena.
Kwa upande wake, TEAGTL inaendelea na uwekezaji wa Shilingi bilioni 410.4 unaohusisha ukarabati wa miundombinu, maboresho ya gati namba 8 hadi 11, ununuzi wa mitambo mipya na usimikaji wa mifumo ya kisasa ya TEHAMA.
Uwekezaji huo umeleta mafanikio makubwa, ikiwemo ongezeko la shehena hadi tani milioni 27.7 katika mwaka wa fedha 2024/2025, sawa na ongezeko la asilimia 17 ikilinganishwa na mwaka uliotangulia.
Katika kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba 2025, bandari ilihudumia tani milioni 16.7, ongezeko la asilimia 30 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2024.
Aidha, muda wa kuhudumia meli za makasha umepungua kutoka wastani wa siku 30 hadi siku 6, hatua iliyopunguza gharama za biashara. Uwekezaji huo pia umechangia kutoa ajira 764 za moja kwa moja hadi Juni 2025, pamoja na maelfu ya ajira zisizo za moja kwa moja kwa madereva, mawakala wa forodha na wafanyakazi wa kutwa.
Bw. Msigwa ameongeza kuwa ushirikiano na wawekezaji hao umeiwezesha TPA kupunguza gharama za uendeshaji kwa wastani wa asilimia 57 na kuongeza uwiano wa faida kutoka asilimia 66 hadi 78. Hali hiyo imeongeza makusanyo ya kodi ya forodha hadi Shilingi trilioni 12.33 katika mwaka 2024/2025, sawa na ongezeko la asilimia 17.
Kwa upande wa miradi inayoendelea, TPA inatekeleza ujenzi wa gati na matanki 15 ya kuhifadhi mafuta yenye uwezo wa lita 378,000 kwa wakati mmoja, ambapo utekelezaji umefikia asilimia 35. Pia kuna mradi wa uboreshaji wa Gati la Malindi lenye urefu wa mita 500, pamoja na miradi ya uboreshaji wa Gati Na. 8–11 na upembuzi yakinifu wa Gati Na. 12–15.
Kadhalika, Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) inaendelea na mradi wa ujenzi wa reli ndani ya Bandari ya Dar es Salaam (MGR, SGR na TAZARA), ambao ukikamilika utaongeza uwezo wa kuhudumia hadi TEUs 480,000 kwa mwaka na kuongeza usafirishaji wa mizigo kwa reli kutoka asilimia 2 hadi asilimia 12.
Kwa ujumla, maboresho hayo yameifanya Bandari ya Dar es Salaam kuwa kichocheo kikuu cha biashara, uwekezaji na maendeleo ya uchumi wa Tanzania na nchi jirani.
Maboresho mengine pia yamefanyika katika bandari mbalimbali ikiwemo mradi wa ujenzi wa bandari ya Kisiwa Mgao Mtwara, maalum kwa ajili ya kuhudumia shehena ya mzigo mchafu (Dirty Cargo) kama vile Makaa ya Mawe na Saruji.
Amesema Mkandarasi anaendelea na utekelezaji wa mradi huu ambao hadi sasa umefikia asilimia 18 ya utekelezaji.
Hali kadhalika ujenzi wa upanuzi wa bandari ya Bukoba, ambao ulihusisha ujenzi wa gati ya kuhudumia shehena ya magari (RO-RO) na meli, kizuia upepo (wind breaker), ujenzi wa eneo la maegesho ya magari pamoja na ujenzi wa jengo la abira. Bandari nyingine ni pamoja na upanuzi wa bandari ya Kemondo uliokamilika kwa asilimia 100, ujenzi wa bandari ya Mwanza North ( asilimia 80), huku kazi kama hizo zikiendelea katika bandari nyingine ikiwemo bandari za Kigoma, Tanga na Mbamba Bay.
Mwisho.
EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"